FOLLOWERS

Sunday, July 15, 2012

SOMA : BARUA YA ADO SHAIBU KWA PROFESA ISSA SHIVJI

Profesa Issa Shivji

BARUA NDEFU KWA KOMREDI PROFESA ISSAGULAMHUSEIN SHIVJI-(1)
S.L.P kijiji cha Namasakata,
Wilaya ya Tunduru.
Kwako Komredi Profesa Issa Shivji,Shikamoo! Ni matumaini yangu u mzima wa siha njema na unaendelea vyema na harakati za kutuamsha wanyonge tuliolala usingizi fofofowakati rasilimali na utajiri wetu ukipokwa na mabeberu mamboleo kwa kushirikiana na ‘’makuwadi wa soko huria’’ kama alivyowaita swahibu wako mpendwamarehemu profesa chachage(Mungu ailaze roho yake ya kizalendo mahala pema peponi).
          Pia nichukue fursa hii adhimu kukupongeza kwa jinsi unavyotumia kalamu yako kutukomboa kifikra sie ‘’wasakatonge’’ tulio kwenye kiza totoro.Naamini bado unakumbuka nasaha za  mwalimu Nyerere alivyowaasa wanazuoni tarehe 27 June 1966 kwenye kongamano la wanazuoni pale chuo kikuu cha Dar es salaam(UDSM) kwamba jukumu kuu la mwanazuoni wa chuo kikuu ni kuutafuta ukweli;kuuzungumza kadiri anavyouona na kuusimamia kwa uthabiti bila kujali gharama yake. Je na wewe upo tayari kuuzungumza na kuusimamia ukweli mpaka mwisho wa dahari?
Kwa hakika nafahamu kuusimamia ukweli kuna gharama kubwa.Lakini nina hakika hakuna jipya linaloweza kumwandama mzalendo yeyote ambalo wasemakweli wengine duniani hawajalipitia. Wanatheolojia wanatujuza kwamba ‘’hakuna jipya chini ya jua’’.Kwa hakika ipo gharama ambayo kila msemakweli duniani anapaswa kuilipa!
        Ni hatari gani inayoweza kumkabili msemakweli hapa duniani kushinda dhoruba ya mlipuko garini iliotupokonya kipenzi chetu Walter Rodney na unyama wa maharamia wa kenya waliomuangamiza komredi Tom Mboya kwa sababu ya uchu wa madaraka? Nakuuliza profesa! Ni vioja gani vinaweza kumsibu mtu kushinda vitimbi vya rais Mobutu Sese Seko kwa Profesa Wamba Dia Wamba na vile vya raisi Obote kwa komredi Nabudara Wadada?Au kuna shubiri chungu namna gani anayoweza kuinywa  mwanazuoni mzalendo kupita uchungu wa korokoroni aliyopitia Ngugi wa Thiong’o na masaibu yaliyomuandama mwana-umajumuhi wa Afrika Dr Osagyefo Kwame Nkurumah?
    Nijibu Profesa.Nijibu komredi!Kuna changamoto gani mnaweza kuipata sasa kuliko zile mlizopitia zama za harakati zenu za University Students African RevolutionaryFront(USARF) wewe na makomredi wenzio kina Profesa Karim Hirji,Henry Mapolu na Liundi pale chuo kikuu Mlimani?Alas!,niwie radhi;nilitaka kuwasahau kina Yoweri kaguta Museveni,Zakia Hamdan Meghi na Omari Ramadhani Mapuri!Kuna watu huku mtaani eti wanaona hawa makomredi niliotaka kuwasahau wamesaliti kile mlichopigania miaka ya sabini.Na wewe unaamini hivyo?
Karibuni umewahi kutufunda kuhusu thamani ya kalamu ya mwanazuoni(Rejea kitabu chako cha Insha zaMapambano Ya Wanyonge).Ulisema kwamba silaha pekee ya mwanazuoni ni kalamu yake na kwamba ni lazima mwanazuoni atumie kalamu yake kwa uthabiti kila anapopata nafasi kuwasemea wanyonge wasio na sauti hususani wakulima na wafugaji(Naomba unipe ruksa niongeze ‘’na machingawa Tandika, Ubungo na kwingineko Tanzaniawanaofurushwa na wanamgambobila ya kuelekezwa pa kwenda!”).
        Binafsi sina maneno toshelezi kuielezea thamani ya kalamu ya mwanazuoni wa wanyonge zaidi ya sifa zilizotolewa na Kajubi kwenye Shairi lake la You write(Rejea kitabu cha Summons:Poemsfrom Tanzania).Inanilazimu kufasili kwa Kiswahili kwa sababu nakala ya barua yako nimeituma kwa umma wawanyonge  wa uswahilini na vijijini:wanyonge ambao mfumo wetu wa elimu umewafanya kuwa wahitimu wa shule za kata wasioweza kuunganisha hata sentesi tatu za kizungu!kajubianamsifia msomi wa wanyonge kwa maneno yafuatayo;
You weep with them
    Unalia pamoja nao(wanyonge)
You sigh with them
Unahema nao(wanyonge)
You suffer with them
Unataabika nao(wanyonge)
But you lift high
Lakini unainua juu
Thebanner of their struggle
                  Bendera ya harakati yao
 With your sacred pen
Kwa peni yako takatifu!
Naam!hayo siyo maneno yangu. Hayo ni maneno ya Kajubi kuhusu msomi wa wanyonge.wanyonge wakiteseka,na yeye anahisi kuteseka;wakihema na yeye anahema;wakilia na yeye anabubujikwa machozi! Ndiyo, ni kupitia kalamu yake iliyotukuka ,bendera ya harakati za wanyonge  inainuliwa juu zaidi na kupepea kuadhimisha ushindi wa umma wa walalahoi.Kwa kweli kajubi alikuwa anawazungumzia waandishi kama wewe, chinua Achebe, wole Soyinka na Ngugi wa Thiongo ;waandishi wa wanyonge.
Kwa hakika beti hizi za kajubi zinawahusu waandishi sampuli ya komredi Abdilatif Abdallah. Si unakumbuka huyu bwana alipowekwa gerezani na Mzee Jomo Kenyata kwa kuhoji Kenya inakokwenda? Je alitokwa na machozi?Gereza lilimkatisha tamaa? La hasha! Aliendelea kuandika kazi zake za kiukombozi akiwa jela kwa kutumia karatasi za chooni!(toilet paper)
Sasa turudi kwenye barua yangu. Kwa kweli asili ya barua yangu ni historia ndefu.Ili kuelewa vyema usuli wake, inanipasa nirejee nyuma kidogo.Miaka kadhaa nyuma nikiwa sekondari, nilipata bahati ya kusoma, kusimuliwa na kutizama habari kuhusu weledi wa wahadhiri wa UDSM. Na kwa kweli baada ya kuja chuoni, nimejionea maprofesa na madaktari wa falsafa waliobobea kwenye fanimbalimbali.
     Wakati ule wa sekondari nilivutiwa sana na habari ya Profesa Haroub Othman, Profesa Rwekaza Simpho Mkandala na Wewe.Kwa bahati mbaya,mauti yalitupokonya profesa Haroub Othman hata kabla sijamuona.Hata Profesa mkandala hakuwa tena kwenye taasisi ya utafiti wa siasa na Demokrasia-REDET.Nilimkuta ametingwa na majukumu ya utawala wa chuo.Mwenyewe amewahi kutueleza kwamba kiutawala, ana malengo(objectives) matatu.Mosi,kuiendeleza UDSM. Lengo lake la pili ,anasema, ni kuiendeleza UDSM.lengo lake la tatu pia ni kuiendeleza UDSM.Ndiyo; anasema hana malengo zaidi ya kuiendeleza UDSM!
Hata wewe nilikuta umekwishastaafu shughuli za uhadhiri.Sikubahatika kukaa darasani ambamo mbele yake kuna mhadhiri aliyeitwa Issa Gulamhusein Shivji.Mwishowe niliamua kujifariji kwa kufuata kivuli chako kila mahali.Nilinunua vitabu vyako,kuhudhuria makongamano na mihadhara yako mingi.Nisingekosa mhadhara wako kirahisi(labda niwe hoi bin taabani kitandani). Swahibu zangu wa karibu wanajua jinsi nilivyokuwa mnazi wa kazi zako.
       Hivyo basi mimi ni mwanafunzi wako;mwanafunzi nje ya utaratibu rasmi.Kama unavyofahamu,ulimwengu wa wanafunzi umejaa maswali. Wanafunzi wasipododosa na kuuliza maswali basi fahamu hapo  hakuna uanafunzi(bila shaka kuna ububusa au labda wanafunzi wamekuelewa kwa asilimia mia!). Wanafunzi wa yesu walimsonga masihi wa Mungu kwa maswali.Maswahaba walimuandama mtume Muhamad(S.A.W) kwa maswali yakufikirisha.
        Na mimi mwanafunzi wako nina maswali.Barua yangu imejaa maswali;maswali ambayo ningekuuliza darasani kama ningepata bahati ya kufundishwa na wewe.Na kama asemavyo Okot p Bitek(Rejea kitabu chake cha Songs of Lawino and Ocol),’’maswali yanapokosa wa kuyajibu yanaumiza kichwa;yanachoma ndani kwa ndani zaidi ya kichomi!.
      Ni matumaini yangu utavumilia maswali yenye dalili za‘’umbumbumbu’’ kwenye baadhi ya maeneo.Naweza( bila kukusudia) kuuliza maswali kuhusu mambo ambayo umekwisha yatolea ufafanuzi kwenye vitabu,mihadhara na maandiko yako.Kumbuka siyo kazi ndogo kumaliza rundo la vitabu vyako.Pia naweza kukuuliza maswali ya ‘’kijuha’’ hapa na pale.Bila shaka,kwa miongo kadhaa ya huduma yako ya ufundishaji UDSM umevumilia ujuha na vimbwanga vingi vya wanafunzi.Vumilia na vituko vyangu!.
Sasa nianze maswali yangu….
Fuatilia waraka huu kwenye sehemu ya pili itayowajia baada ya siku chache.
Kwa maoni: adoado75@hotmail.com/ado75haki@gmail.com simu:0653619906.




               

11 comments:

Anonymous said...

very interesting...tutapataje sehemu ya pilli?

Anonymous said...

tuletee na sehemu ya pilli mkuu..

Anonymous said...

tunasubiria kwa ha
mu sehemu ya pili

Nivard said...

kaka i real appreciate your contribution towards right and equality. keep it up. god be with you.

Unknown said...

thanx a lot for your comments, i got it from john mnyika group on facebook...so i will try harder to bring you the second part

Hafsa said...

jamani swahiba nimependa kazi yako inshaalah mwenyez mungu atafungua njia kwako na kazi zako

Unknown said...

asante sana hafsa..inshallah mwenyezi mungu atajalia..kazi njema kwako pia

Anonymous said...

I always proud being among your best friend,namshukuru mungu aliyenileta UDSM na kunikutanisha na beloved kaka anayejielewa, i always pray for u kaka,all the best beloved

gabriel batikwisa said...

very gud kaka addo shaib...i believe utakuwa mwandishi mahiri huko mbele..nina hamu sana na sehemu ya pili...tutaipata lini

ado shaibu said...

this is for z blog owner: sehemu ya pili iko tayari.kwa sababu ya kukata kiu ya wasomaji wako ya kufahamu mwendelezo wa barua hii,tuwasiliane kwa kutumia ukurasa wa fb(ado shaibu),e-mail adoado75@hotmail.com, simu:0653619906

Unknown said...

nimefurahi sanaaa...ADO SHAIBU...nakufuata FB..nipate mengi

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...