FOLLOWERS

Friday, August 10, 2012

HOTUBA YA MSEMAJI MKUU WA KAMBI RASMI YA UPINZANI MHE. MCHUNGAJI PETER MSIGWA, (MB) WIZARA YA MALIASILI NA UTALII, KUHUSU MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI KWA MWAKA WA FEDHA 2012/2013

HOTUBA YA MSEMAJI MKUU WA KAMBI RASMI YA UPINZANI  MHE.  MCHUNGAJI PETER MSIGWA, (MB) WIZARA YA MALIASILI NA UTALII, KUHUSU MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI KWA MWAKA WA FEDHA 2012/2013.
1.0 UTANGULIZI
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Kambi rasmi ya Upinzani,nakushukuru kwa kunipa nafasi hii ya kuwasilisha Maoni na Mapendekezo ya Kambi rasmi rasmi ya upinzani bungeni kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa mwaka wa fedha 2012/2013, kwa mujibu wa Kanuni za Bunge Kifungu cha 99(3) na (7) toleo la 2007.
Mheshimiwa Spika, naomba nichukue fursa hii kutoa pole kwa msiba mkubwa wa jirani yangu mama KISILO ambaye amefariki tar 7 Julai na kutokana na majukumu ya kibunge nimeshindwa kuhudhuria mazishi, pia wananchi waliopoteza maisha kutokana na ajali mbaya ya basi la Sabena iliyotokea Tabora ,Mungu aziweke roho za marehemu mahala pema peponi.
Mheshimiwa Spika, Napenda nichukue fursa hii kuwakumbusha wapiga kura wangu wa jimbo la Iringa mjini, Kama nilivyoapa kuilinda na kuitetea katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nitaendelea kusema ukweli bila kujali cheo cha mtu,rangi,kabila wala dini yake kama maneno ya kiongozi wa taifa la India  marehemu Mahatma Ghandhi alivyowahi kutuasa  akisema maneno yafuatayo;
 “….Many people especially ignorant people, want to punish you for speaking the truth, for being correct for being you... Never apologize for being correct or being years ahead of your time, if you are right and you know it, speak your mind even if you are a minority of one, the truth is still the truth”.
Kwa tafsiri ya Kiswahili isiyo rasmi …Watu wengi hasa watu wajinga,wanataka kukuadhibu kwa kusema ukweli,kwa kuwa sahihi,kwa kuwa na msimamo binafsi,Kamwe usiombe radhi kwa kusema ukweli au kwa kuwa mbele ya wakati. Kama upo sahihi na unafahamu hivyo sema, hata kama Ni pekeyako, ukweli utabaki kuwa ukweli.
Mheshimiwa Spika,Dira ya Wizara hii ni kuhakikisha utunzaji endelevu wa maliasili, utamaduni na Utalii na kuhakikisha ushirikishwaji wa jamii zinazohusika, mashirika yasiyo ya kiserikali na kusimamia matumizi ya maliasili kwa faida ya vizazi vya sasa na vijavyo.
Mheshimiwa Spika, hali halisi imeendelea kuwa kinyume chake, Watanzania ndani ya nchi hii, yenye utajiri mkubwa wa misitu na mbuga nyingi za wanyama, milima na mabonde ya kuvutia, wameendelea kuwa maskini hata baada ya miaka 50 ya uhuru wa nchi yao.
Mheshimiwa spika, pamoja na mambo mengine jukumu la wizara hii ni kuandaa sera na mikakati ambayo itaongoza utunzaji endelevu wa maliasili, utamaduni na mazingira. Kuinua na kuongeza aina ya vivutio vya utalii na kuongeza mchango wa sekta hii kwa pato la taifa na uingizaji wa fedha za kigeni.
Mheshimiwa Spika, ni dhahiri wizara imeshindwa kusimamia  sera na mikakati ya kuendeleza maliasili, utamaduni na mazingira kama iliyojiwekea, moja Wizara imeshindwa kuvutia watalii zaidi,  pili imeshindwa kulinda misitu na kuacha misitu ikiteketea, tatu imeshindwa kulinda wanyamapori ambao wameendela kuibiwa na kuuwawa, nne idara ya wanyapori imeendelea kudhoofishwa na kushindwa kutekeleza majukumu yake kama inavyotakiwa hasa kutokana na Waziri mwenye dhamana kuacha nafasi muhimu za maamuzi katika idara hii zikikaimiwa na watendaji mbalimbali ambao wameshindwa kuwa na maamuzi hivyo kuleta urasimu usiokua na tija kwa taifa, na tano Wizara kushindwa kutunza mlima Kilimanjaro ambao theluji imeendelea kuyeyuka huku hakuna mkakati wa makusudi kuokoa mlima huo.
2.0 SEKTA NDOGO YA WANYAMAPORI.
Mheshimiwa Spika, Mwalimu J.K. Nyerere aliwahi kusema, nanukuu; “Uhai wa wanyamapori ni jambo linalotuhusu sana sote katika Afrika. Viumbe hawa wa porini, wakiwa katika mapori wanamoishi, sio muhimu tu kwa ajili ya kuajabiwa na kuvutia lakini pia ni sehemu ya maliasili yetu na pia ndio mustakabali wa maisha yetu ya baadaye. Kwa kukubali dhamana ya wanyamapori wetu tunatamka kwa dhati kwamba tutafanya kila tuwezalo kuhakikisha kwamba wajukuu wa watoto wetu wataweza kufurahia urithi huu mkubwa na wa thamani adimu.”
Mheshimiwa Spika, Serikali hii ya CCM siyo tu imeshindwa kuwalinda wanyama wake na vivutio vya asili bali pia imeshindwa kuwalinda raia wake na kwenda kinyume kabisa na dhana ya Mwalimu Nyerere. Tangu tulipopata uhuru,tumeshuhudia raia wengi kupoteza maisha kwa kuuwawa na ajali mbalimbali ambazo zimesababishwa na Serikali dhaifu na zembe ya CCM mfano meli za Mv Victoria,  Mv Skagit,Mv Spice Islander, mabasi na pikipiki na matukio mengine kadha wa kadha ambayo tukiyaorodhesha hapa muda hautotosha. Kama vile haitoshi watanzania na dunia nzima tumeshuhudia wanyama wakiporwa na kusafirishwa nje ya nchi, tembo kuuwawa kwa kasi kubwa huku Serikali hii ikiendelea kukaa kimya na kutokua na majibu wala mikakati hasa ya kukabiliana na ujangili.
Mheshimiwa Spika, kutokana na utamaduni uliojengeka na serikali ya CCM ya kutegemea misaada na kuwa ombaomba katika mataifa mbalimbali kinyume na wosia aliotuachia hayati Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere kwamba nchi maskini haiwezi kuendelea kwa kutegemea misada kutoka nchi za nje,hali hii imeendelea kulifanya Taifa kushindwa kulinda rasilimali zake na kujikuta likiendelea na utamaduni wa kuomba hata vile tulivyojaliwa na Mwenyezi Mungu kuwa navyo,mfano hivi karibuni Tanzania na Dunia nzima imeshuhudia Waziri wa Maliasili na Utalii,Mh Balozi Hamis Kagasheki akifurahia kupeana mikono na Balozi wa Uingereza akipokea Faru watatu kutoka uingereza kana kwamba ni jambo la kujivunia huku Tanzania ilipaswa kuuza na kugawa Faru kwa nchi hizo za kigeni.
Mheshimiwa spika, takwimu zinaonesha mwaka 2008 hadi mwaka 2012 Mei  taifa hili limekwisha poteza Tembo takribani 881,udhaifu huu wa ulindaji wa wanyama hawa umetokana na serikali kutotambua umuhimu wa kulinda rasilimali hizi na kuweka kipaumbele katika kuhakiki usalama wa wanyama hao, kitu ambacho ni mshangao kwa mfugaji anaetegemea kupata mazao pasipo kuwalisha mifugo wake.
Kambi rasmi ya Upinzani, inataka kujua serikali imechukua hatua gani mpaka sasa kwa wale wote waliohusika kwa njia moja ama nyingine na vifo vya wanyama hawa na kuliingizia taifa hasara kubwa.
2.1  WATUMISHI IDARA YA WANYAMAPORI
Mheshimiwa Spika , mahitaji halisi ya watumishi katika idara ya wanyamapori ni watumishi 4,588 huku idara ikiwa na watumishi 1,044,hivyo kufanya  idara kuwa  na upungufu wa watumishi 3,544 sawa  na upungufu wa asilimia 77,  matokeo yake ni kupelekea askari mmoja alazimike kufanya doria katika eneo la kilometa za mraba 159.75 badala ya kiwango kinachokubalika kimataifa cha kilometa za mraba 25 kwa askari mmoja. Kambi ya Upinzani inaitaka serikali kutoa ufafanuzi ni jinsi gani askari hawa wanaweza kukabiliana na tatizo la ujangili katika hifadhi zetu za wanyamapori? Na pia ni mkakati upi uliopo Serikali kukabiliana na upungufu wa watumishi katika Idara ya Wanyamapori?
Mheshimiwa Spika, mtalaamu wa maswala ya ujangili wa kimataifa Dr Donald Antony Mwitulubani wa idara ya Geografia ya chuo kikuu cha Dar Es Salaam anasema katika mojawapo ya mada zake; “ Majangili hutumia udhaifu uliopo katika taratibu za usafirishaji au uingizaji na kukosekana kwa ushirikiano baina ya vyombo vya kutekeleza sheria kitaifa na kimataifa,hutumia njia nyingi kuepuka kujulikana na kukamatwa, hushirikiana na majangili wengine waliojizatiti zaidi kufanya ufisadi, kutoa rushwa, kuingiza fedha chafu, madawa ya kulevya kumiliki na kutumia silaha za moto”.
Ni dhahiri kwa maneno haya kuwa idadi ndogo ya askari iliyopo itaiwia vigumu kuweza kukabiliana na majangili hawa kutokana na nguvu kubwa walionayo na mitandao iliyopo pamoja na serikali kutokuwa na nia ya dhati ya kukabiliana na ujangili uliokithiri.
3.0 SHUGHULI ZA UWINDAJI
Mheshimiwa Spika, suala la uwindaji kwa kuzingatia sheria bado limeonekana kuwa na mapungufu kwa upande wa Serikali katika kusimamia kwa ukamilifu, sheria na taratibu zinataka DGO’s (District Game Officers) kuwepo wakati wa kutekeleza shughuli ya uwindaji. Limejitokeza tatizo la uwindaji kukiuka taratibu katika kitalu cha uwindaji cha Loliondo pindi Mfalme wa Uarabuni anapokuwa akifanya uwindaji pasipo kuwepo kwa game officers kwa maelezo ya taratibu za kiitifaki, ambapo game officers wameshindwa kutoa maelekezo ya aina ya wanyama wa kuwindwa hivyo kupelekea wanyama kuwindwa ovyo pasipo taratibu za kitaalamu kufuatwa, kwa mfano wanyama wajawazito nk.
Mheshimiwa Spika,kwa mujibu wa kanuni ya tano ya Kanuni za ukamataji wanyama inamtaka mmiliki wa kibali cha kukamata wanyama kuripoti kwa Afisa Wanyamapori wa wilaya husika kabla na baada ya ukamataji kufanyika kwa lengo la kumuonyesha eneo la ukamataji, kusimamia zoezi la ukamataji na baadye kusaini na kuweka muhuri katika hati ya ukamataji (capture permit).
Mheshimiwa Spika, hata hivyo,masharti ya kanuni hii yameonekana kupuuzwa pale wanyama wanapokamatwa,mfano maafisa kutoka kikosi cha kuzuia Ujangili arusha(KDU), maafisa kutoka TAWIRI, maafisa kutoka CITES,Arusha na mwakilishi wa kampuni ya Gumbo Reptiles wamekua wakikamata bila kutoa taarifa kwa mamalaka za wilaya za Monduli.
Mheshimiwa Spika,Kambi rasmi ya Upinzani inaitaka Serikali kuthamini mali za umma na sio kuendeleza utamaduni wa kigeni wenye  kutumia rasilimali zetu bila kufuata taratibu tulizojiwekea kama taifa. Pia, Kambi ya Upinzani inaitaka Serikali kutoa maelezo ni hatua zipi za kisheria zinazochukuliwa dhidi  ya tuhuma hizi na mikakati yake katika kutoa adhabu kali ili kuwa fundisho kwa wavunjaji wa Sheria na Kanuni za uwindaji nchini.
3.1  ELIMU YA UWINDAJI WANYAMAPORI.
Mheshimiwa Spika, Sera ya taifa katika uwindaji imeainisha suala la kuweka kipaumbele cha uwindaji kwa wawekezaji wa ndani hivyo kutoa kipaumbele kwa watanzania kushiriki katika uwindaji wa wanyamapori. Suala la uwindaji linahitaji taaluma ya uwindaji na taarifa rasmi za masoko, na kutokana na mahitaji hayo watanzania wengi kutokuwa na vigezo vya kushiriki katika uwindaji huo,Kambi rasmi ya Upinzani inaitaka serikali kutoa elimu ya kutosha kwa watanzania ili kuwawezesha kushiriki vema katika kukuza uchumi kwa kushiriki moja kwa moja  katika shughuli za uwindaji wa wanyamapori.
3.2  Kuongezeka kwa idadi ya vitalu vya uwindaji.
Mheshimiwa Spika,Katika kipindi kinachomalizika,  idadi ya wanyama ilikuwa kubwa zaidi kulinganisha na idadi ya sasa ambapo tafiti mbalimbali zimeonyesha kuwa wanyama wamekuwa wakipungua kadiri siku zinavyokwenda. Pamoja na ukweli huu idadi ya vitalu imeongezeka na wakati huo huo idadi ya wanyama wanaoweza kuwindwa kwa mwaka haijaongezeka ( quota setting) , hii ina maana kuwa wanyama wengi zaidi watawindwa kutokana na wingi wa makampuni yalivyo na hivyo kwenda kinyume kabisa na Sera ya  Taifa ya uhifadhi wa wanyama pori.
Kambi ya Upinzani , inataka kujua vigezo vilivyotumika katika kuongeza idadi ya vitalu bila kuzingatia uhalisia na uwepo wa wanyama.
Mheshimiwa Spika, Pia  vitalu vingine vimegawanywa bila kuzingatia ikolojia ya eneo husika na haswa wakati wa kuweka mipaka baina ya vitalu hivyo, hii nayo ni tishio kwa ikolojia na wanyama wanaoishi eneo husika lililogawanywa bila kuzingatia uhalisia huu wa kitaalamu kwa mfano kugawa eneo la kuwinda Mamba au Viboko ambao wanakaa eneo moja la maji kwa kampuni mbili tofauti wakati wanyama hawa wanahama kulingana na msimu wa mwaka ni jambo la ajabu kabisa.
Kambi ya upinzani, tunataka kupata maelezo ya kina juu ya ugawaji huu kama ulizingatia vigezo na kama sivyo nini msimamo wa serikali katika hili kwa sasa.
3.3 Ugawaji wa Vitalu Kutokuzingatia Sheria ya Uhifadhi Wa Wanyamapori .
Mheshimiwa Spika,Hii inatokana na ukweli kuwa kwenye baadhi ya maeneo ambayo vitalu vimegawanywa na kuongezwa na kugawiwa kwa makampuni mbalimbali, kulienda kinyume na sheria ya uhifadhi wa wanyama pori kifungu cha 16 (Wildlife Conservation Act 2009 No.5 of 2009)
Mheshimiwa Spika, Kwa mfano ugawanyaji wa vitalu vilivyopo eneo la Ziwa Natron umeenda kinyume na kifungu 16 (4 na 5). Vifungu hivi vinatamka wazi kuwa Waziri hatagawanya eneo kwanza kabla ya kushirikisha Serikali za vijiji kwenye eneo husika na kutangaza maeneo hayo kwenye Gazeti la Serikali, pamoja na kifungu hicho bado Waziri aligawanya eneo hilo kutoka vitalu viwili vya awali hadi kuwa vinne bila kuzingatia takwa hili la kisheria.
Mheshimiwa Spika,Athari kubwa ya jambo hili ni kuwa wakati Waziri amegawa eneo hilo kwa kampuni tofauti ameshindwa kuzingatia ukweli kuwa vijiji husika vilikuwa tayari vimeshasaini mikataba na kampuni ya Wengert Windrose Safaris (WWS) na kuwa walishakubaliana kuanzishwa kwa WMA kwenye eneo hilo na hivyo aligawanya eneo ambalo hakuwa na mamlaka nalo kisheria kwa wakati huo .
Kambi ya Upinzani,inataka kupata majibu ni kwanini wizara inashiriki kuvunja sheria zilizotungwa na Bunge hili.
3.4 Mapungufu ya Ugawaji wa Vitalu vya Uwindaji kwa kipindi cha 2013-2018
Mheshimiwa Spika, Kifungu cha 38(14) cha Sheria ya Wanyama Pori kinamruhusu mtu yeyote aliyekwazwa na maamuzi ya Waziri kumwandikia waziri kuomba uamuzi huo kupitiwa upya. Kama tujuavyo, wadau wengi walioathirika na maamuzi ya waziri waliomba uamuzi wa Waziri aliyepita kuangaliwa tena. Kifungu 38(15) kinaendelea kueleza kwamba baada ya maombi ya kutazama upya maamuzi yaliyopita, Waziri atawasilisha maombi hayo kwenye Kamati ya Ushauri ya Ugawaji wa Vitalu vya Uwindaji kwa ajili ya kupata maoni na mapendekezo ya Kamati. Baada ya kupokea maoni na mapendekezo ya Kamati.
Mheshimiwa Spika,bado dhana ya utawala bora inashindwa kufikiwa na Serikali katika kutekeleza majukumu yake katika wizara ya maliasili na utalii hasa kwa kuendelea kuwa mgawaji wa maeneo ya vitalu vya uwindaji wa kitalii kama ilivyopendekezwa kabla kuwepo na mamlaka tofauti itakayotekeleza jukumu hilo kisheria na Wizara kubaki kuwa msimamizi wa utekelezaji wa Sera.
Kambi ya upinzani, inaitaka Serikali kuona umuhimu wa kubaki kuwa msimamizi wa utekelezaji wa Sera ili kuleta tafsiri sahihi ya utawala bora kiutendaji katika swala la mgawanyo wa madaraka,hii itaweza walau kuijengea heshima serikali hii dhaifu ya CCM ndani na nje ya nchi katika kuwaletea wananchi mfumo sahihi wa utawala bora kwa kutenda.
3.4 Uwazi  katika mchakato wa kutenga vitalu vya uwindaji
Mheshimiwa spika, Kifungu cha 38(11) cha Sheria ya Wanyama Pori  kinaeleza kwamba mchakato wa kutenga na kugawa vitalu vya uwindaji utakuwa wa wazi, unaoweza kuhojiwa, wenye kuzingatia haki, usawa na wa maridhiano. Waziri hakuweza kutoa sababu kwa wadau ni kwanini wadau walinyimwa vitalu walivyokuwa wameomba. Wakati wadau walipoomba taarifa kuhusu vitalu vya uwindaji waliambiwa kwamba taarifa hizo ni za siri. Hii sio haki kwa mujibu wa kifungu 38(11) cha Sheria ya Wanyama Pori ambacho kinamtaka Waziri kusimamia mchakato huo kwa uwazi kadiri iwezekanavyo ili kudumisha utawala bora.  Kambi rasmi ya Upinzani inahoji uwazi wa Waziri katika kutoa taarifa kwa wadau hasa wale waliokosa kwa kigezo cha unyeti wa taarifa hizo huku sheria ikitaka mchakato huo kuwa ni wa uwazi.
3.5 Idadi ya Wanyama katika Eneo la Uwindaji
Mheshimiwa Spika, Sheria inamtaka Waziri kutoa taarifa za kina na ramani zinazoonesha eneo la uwindaji na mipaka yake kwa vipindi vya uwindaji baada ya Sensa ya Wanyama itakayokuwa imefanywa na Wizara. Kifungu cha 44(1) cha Sheria ya Wanyamapori kinaeleza kwamba kwa madhumuni ya kumshauri Mkurugenzi namna ya kuanzisha eneo la uwindaji, Waziri atateua kamati ya wajumbe wenye ujuzi na uzoefu wa masuala ya Usimamizi wa Wanyamapori. Kamati hii haikuundwa.
Mheshimiwa Spika, Kambi rasmi ya upinzani imeona kuwa jambo hili lilisababisha ugawaji holela wa vitalu vya uwindaji na kuacha maeneo mengine bila wanyama. Udhaifu huu umesababisha wadau kutegemea sensa ya wanyama iliyofanywa na mipaka ya vitalu vya uwindaji iliyofanya na watu binafsi kwa uzoefu wao. Kambi rasmi inaitaka Serikali, kwa kupitia waziri wake kutoa majibu juu ya usimamizi wake katika kuhakikisha Sheria zinafatwa, na ni vipi ugawaji wa vitalu haukuhusisha kamati kama Sheria inavyoainisha hivyo kufanya zoezi hili la ugawaji wa vitalu kuwa batili.
Mheshimiwa Spika, Waziri alifanya maamuzi lakini maamuzi hayo kwa kiasi kikubwa hayakuzingatia maoni na mapendekezo ya Kamati. Hii ilithibitika kutoka katika taarifa iliyopita iliyosomwa na kamati ya Bunge ya Ardhi Maliasili na Mazingira. Ikitokea wadau hawa ambao hawakuridhika wakaamua kuupinga uamuzi wa Waziri wa kugawa vitalu vya uwindaji kwa kipindi cha 2013-2018 kama ulivyokiuka kifungu 38(16), Serikali itashindwa vibaya na itasababisha matumizi makubwa ya fedha kwa ajili ya kulipa fidia kampuni husika.
3.6  Utafiti na Maendeleo ya Maeneo ya Uwindaji
Mheshimiwa Spika, Kwa mujibu wa kifungu cha 37 cha Sheria ya Wanyama Pori Waziri alitakiwa kuagiza usimamizi wa mazingira na ukaguzi wa miradi ya mazingira au shughuli mbalimbali zinazofanywa katika vitalu mbalimbali vya uwindaji.  Ukaguzi huo haukufanywa na Waziri kama Sheria ilivyomtaka.
Mheshimiwa Spika,Zaidi ya hilo, Kanuni ya 3(1) inasema kwamba, Mkurugenzi ataanzisha maeneo katika Hifadhi za Wanyama Pori, maeneo tengefu ya wanyama pori na maeneo mengine nje ya maeneo yanayolindwa ili yageuzwe kuwa vitalu vya uwindaji ili mradi kwamba vitalu vya uwindaji vilivyotengwa katika maeneo ya usimamizi wa Wanyama Pori vitaidhinishwa pamoja na Mpango wa Kanda wa Usimamizi wa Rasilimali au Mpango Mkuu  wa Usimamizi wa maeneo husika ya Wanyama Pori. Mipango hii ya usimamizi wa rasilimali wa Kanda na Mpango Mkuu wa Usimamizi haijatekelezwa na Waziri kama kifungu cha 34(2) cha Sheria kinavyoelekeza.
Mheshimiwa Spika, Kwa mujibu wa kifungu 38 (10)  cha Sheria ya Wanyama Pori, mambo yote yanayohusu madaraja , ukubwa na ubora wa vitalu vya uwindaji yameainishwa katika kanuni.
Taarifa hizi zilitolewa chini ya Kanuni za Uwindaji wa Kitalii za 2010 kwa njia ya jedwali dogo kwa kuonesha tu namba ya daraja na vitalu vya uwindaji vilivyokuwa katika madaraja hayo. Waziri hakueleza ni kwanini madaraja kadhaa ya vitalu vya uwindaji yalitengwa maalumu kwa kipindi cha uwindaji kutoka 2013 -2018. Taarifa pekee iliyotolewa ilihusu ukubwa wa kitalu cha uwindaji lakini taarifa ya sababu za kuchagua kitalu cha uwindaji na ukubwa wake hazikutolewa.
3.8 Ajira Kutolewa kwa wageni kutoka nje ya Nchi.
Mheshimiwa Spika,Kutokana na kukosekana kwa wataalamu waliobobea kwenye sekta hii nchini mwetu ,kumesababisha nafasi  nyingi za ajira kutolewa kwa wataalamu kutoka nje ya nchi na hivyo vijana wa kitanzania wenye sifa stahiki wanajikuta wanakosa fursa za kupata ajira za kitaalamu kwenye sekta hii na kubakia na ajira za kawaida kama kuwinda na kuhifadhi tuu .
Mheshimiwa Spika, Hali hii inapelekea fedha nyingi za kigeni kulipwa na kupelekwa nje ya nchi na hivyo kulikosesha taifa fedha za kuendeleza miradi mingine mbalimbali na hali hii imesababishwa na ukosefu wa vyuo vya kutoa elimu ya juu kwenye masuala ya uwindaji nchini mwetu.
Mheshimiwa Spika, Umakini wa kimataifa umeelekezwa kwa wanyama wa Tanzania kwa sababu ya uhifadhi wa bioanuai, lakini hapa kwetu Tanzania suala katika usimamizi wa wanyamapori limeendelea kuwa ni tatizo kubwa hivyo kuendelea kudhoofisha maendeleo ya kijamii na  kiuchumi.
Mheshimiwa Spika, itakumbukwa Kipindi cha miaka ya 1990 Wizara ya Maliasili na Utalii Tanzania ilifanya tathmini ambayo ilihitimisha kwamba,“Ni muhimu kwa uhifadhi wa wanyamapori hapo baadaye kwa hapa Tanzania wananchi waishio pamoja na wanyamapori wapatiwe mafao ya moja kwa moja yatokanayo na wanyama”.
Mheshimiwa Spika, Pamoja na gharama hii na uwezo wake wa kiuchumi kwa taifa na jumuia za vijijini zilizo jirani na maeneo ya hifadhi ya wanyamapori, sekta ya wanyamapori haijaweza kuendelezwa kufikia uweza wake kikamilifu kutokana na matatizo yafuatayo:
Kutokuwepo kwa Sera ya Wanyamapori iliyo wazi.
Kushindwa kwa uhifadhi wanyamapori na kushindana na  namna nyingine za matumizi ya ardhi, hasa katika jamii za vijijini.
Kutokuwepo kwa mwamko juu ya uhifadhi wa wanyamapori miongoni mwa wapangaji wa mipango na maafisa wenye mamlaka, na hivyo basi, suala la ardhi na wanyamapori kupewa uzito mdogo sana wakati wa upangaji mipango.
Kuongezeka kwa ujangili kwa kasi kubwa na biashara isiyo halali kunakosababishwa na udhaifu katika utekelezaji wa Sheria na Sera zilizopo.

Mheshimiwa Spika, Katika mabadiliko yanayotokea ya kiikolojia, kiuchumi na kijamii katika muktadha wa kitaifa na kimataifa,Kambi rasmi ya Upinzani inaitaka Serikali kuimarisha sekta ya wanyamapori kwa kuzingatia yafuatayo;


Kuweka sera madhubuti za uendeshaji wa shughuli za wanyamapori, na kushiriki kikamilifu katika uendeshaji na usimamizi wa rasilimali za wanyamapori nchini kote.

Kuweka na kuwezesha kuwepo kwa mazingira halali na ya kisheria yatakayoziwezesha jamii za vijijini na sekta binafsi kushiriki katika shughuli kwenye  mapori ya akiba.
Kuweka utaratibu endelevu utakaosimamia na kuhakikisha kwamba kunaendelea kuwepo maeneo yaliyohifadhiwa ambapo wanyamapori na maeneo mengine ya asili yataendelea kuhifadhiwa.
Kupiga vita matumizi haramu ya wanyamapori.
Kuwawekea wafanyakazi wa idara ya wanyamapori kanuni za maadili ya kazi zao.
Kuanzisha mfumo wa utunzaji wa habari zinazohusu wanyamapori.



3.9 UWINDAJI, UFISADI NA  UKIUKWAJI WA SHERIA  ZA MATUMIZI YA ARDHI


Mheshimiwa Spika, kama tulivyosema kwenye hotuba ya Ardhi leo tunarudia tena kuwa, Kwa muda mrefu sasa Ardhi ya Tanzania imegeuzwa shamba la bibi na kikundi cha mafisadi! Kambi ya upinzani imeshuhudia mkataba ulioingiwa baina  ya kampuni  za Uranium  resourses  PLC , Western Metals Limited  na Game frontiers  of Tanzania Limited . Mkataba ambao umetengenezwa na kampuni ya kitanzania ya REX ATTORNEYS. Na ulisainiwa tarehe 23.3.2007.


Mheshimiwa Spika, Mkataba husika,ambao vipengele vyake vinaainisha kwamba unatakiwa uwe wa SIRI unaihusu kampuni ya uwindaji, inayofahamika kwa jina la Game frontiers  of Tanzania Limited  inayomilikiwa na Bwana Mohsin M. Abdallah  na ndugu Nargis M. Abdallah .   Kampuni hii ya uwindaji, imeingia mkataba na kampuni mbili za kigeni, za kufanya utafiti wa uchimbaji wa madini ya Uranium katika kijiji cha Mbarang’andu  kwa malipo yafuatayo:-


Malipo ya $ 6,000,000/- za kimarekani, ambazo zitalipwa kwa  awamu mbili ya malipo ya $3,000,000. Malipo ya kwanza yatafanyika  pale uzalishaji wa urani takapoanza.


Malipo ya $ 250,000/- baada ya kampuni za madini kukamilisha utafiti wa madini ya urani na  kupata kibali cha uchimbaji wa madini.


Malipo ya $ 55,000 kila mwaka kama fidia ya kushindwa kufanya biashara na usumbufu unaotokana na shughuli za machimbo kwenye kitalu! Malipo hayo yatafanyika kila tarehe 31 Machi.

 Malipo ya $ 10,000 kwa vijiji vitakavyoathiriwa na utafiti huo wa urani. Malipo ambayo yametokana na makubaliano baina ya kampuni ya uwindani na kampuni za madini!

Mheshimiwa spika,Nimepitia sheria za uhifadhi wa wanyamapori, The wildlife Conservation Act, 1974 (Sheria ya zamani) na Sheria mpya The wildlife Concervation Act, Act no 5 of 2009. Sheria hizi zinamruhusi mtu aliyekuwa na leseni ya uwindaji, kuwinda wanyama tu! Tena wale alioruhusiwa katika leseni ya uwindaji!


Mheshimiwa spika, Halikadhalika, Sheria ya ardhi, ya Mwaka 1999, Sheria namba 4 ya mwaka 1999 na Sheria ya ardhi ya vijiji, sheria namba 5 ya mwaka 1999  inatamka bayana kwamba ardhi inajumuisha vitu vyote vilivyo juu ya ardhi na chini ya ardhi isipokuwa madini au mafuta, Na kwa mujibu wa sheria za Tanzania linapokuja suala la madini, umiliki unatoka kwa mtu binafsi na kurudi serikalini! Na ni Serikali kupitia wizara ya Nishati na Madini ndio pekee yenye mamlaka ya kutoa leseni ya kutafuta madini kwa kampuni za madini!


Mheshimiwa Spika, Kambi ya upinzani inaitaka serikali ilieleze Bunge lako tukufu uhalali wa mkataba kati ya Game Frontiers na Uranium Resourses PLC na Western Metals! Ni sheria ipi inayoipa kampuni ya uwindaji haki ya kualika kampuni ya nje kwenye eneo ambalo haina umiliki kufanya utafiti na hatimaye kuchimba madini hatari kama urani? Nini mustakabali wa watanzania wanaoishi kwenye vijiji vinavyozunguka mbunga hiyo ambao wanaishi maisha yao ya kila siku pasipo kujua kama kuna utafiti wa madini hatari ya urani unaoendeshwa kwa siri kubwa? Ni serikali ya aina gani, yenye uwakilishi mpaka ngazi ya kitongoji na usalama wa taifa mpaka ngazi za chini kabisa za utawala inashindwa kuyaona haya?

Kambi ya Upinzani, Tunasisitiza kuwa, kwa kuwa Kampuni hii ya Game Frontiers Tanzania Limited  imevunja sheria za nchi na ni kinyume na leseni waliyopewa ya kuendesha shughuli za uwindaji ni wakati sasa wa waziri wa Maliasili na Utalii atangaze kuifutia leseni ya uwindaji leo na sio kesho ili iwe fundisho kwa wengine .

4.0 TAARIFA ZA WATUMISHI WA SERIKALI KUHUSIKA NA UJANGILI.


Mheshimiwa Spika, kumekuwepo taarifa za baadhi ya watumishi wa serikali kuhusika katika matukio ya ujangili katika hifadhi za taifa na taarifa za uchunguzi kuzifikia mamlaka za serikali pasipo kuzifanyia kazi huku watumishi hawa ambao ni askari polisi wakitumia magari ya Serikali na magari yao binafsi kusindikiza misafara iliyobeba mizigo ya nyara za Serikali. Kambi rasmi  ya Upinzani inahoji ukimya wa Serikali pale uchunguzi unapothibitisha ushiriki wa baadhi ya watumishi katika ujangili ambapo pamoja na wahusika kufahamika kwa majina bado kumekuwa na udhaifu na ulegelege katika kuwachukulia hatua za kinidhamu na kisheria.


Mheshimiwa Spika, Taarifa kuhusu kupewa dhamana kwenye mahakama ya Serengeti - Mugumu kwa mtuhumiwa aitwaye Bryson Baloshigwa Naftali, mkaazi wa kijiji cha Busunzu, wilaya ya Kibondo, mkoa wa Kigoma ambaye anathibitika kuwa ni  kiongozi  mkuu wa mtandao wa ufadhili wa uwindaji faru na biashara haramu ya meno ya tembo katika maeneo ya hifadhi za Serengeti,Katavi, Tarangire, Ziwa Manyara, Hifadhi ya Ngorongoro pamoja na Mapori ya Akiba kama Ugalla, Rungwe, Moyowosi, Maswa. Kambi rasmi ya Upinzani ina taarifa na ushahidi kuwa nyara zinazopatikana huzisafirisha nje ya nchi kwenda Burundi, Uganda na kwingineko ambapo mtuhumiwa amejitengenezea mtandao mkubwa ulioenea hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, Mtuhumiwa huyo alikamatwa tarehe 11.06.2012 kwa kesi namba MUG/IR/1330/2012 akiwa kwenye kituo cha Polisi cha Kibondo, baada ya kufikishwa Mugumu,alilegezewa masharti ambapo mtuhumiwa huyo pamoja na mwenzake Kama Yohana Tika (mpigaji Tembo maarufu mkoani Kigoma na muwakilishi mkuu wa Bryson katika ujangili) walifunguliwa kesi tofauti na tuhuma zao ambayo ni kuazimisha silaha, kesi ambayo ina urahisi wa kupata dhamana,na wengine kufunguliwa kesi ya ujambazi kutumia silaha “armed robbery”,  kwa baadhi ya washirika wake wasio na ushawishi wa fedha.
Mheshimiwa Spika,Kambi rasmi ya Upinzani inasikitishwa na utendaji wa mamlaka za serikali na serikali yenyewe,pamoja na kuwepo kwa taarifa hizi Serikali imeendelea kuwaacha huru watuhumiwa hawa bila kuchukua hatua madhubuti na kuendelea na kuzimaliza maliasili za nchi hii.
Mheshimiwa Spika ulegevu huu wa Serikali ukiambatana na mazingira ya rushwa ulithibitika mnamo tarehe 09.07.2012 mtuhumiwa  Bryson alipochukuliwa rumande, kwa kibali maalum “removal order” na kufikishwa Mahakamani kisha kupata dhamana, na inasemekana kuwa alitakiwa kurudishwa Kigoma kwa gharama za Serikali kama alivyoletwa hapo Mugumu kwa escort ya Polisi. Kwa kawaida mtuhumiwa huyo alipaswa kufikishwa mahakamani tarehe 15/7/2012 kwa kesi yake kutajwa kwa mara nyingine kufuatia taratibu za kimahakama.
Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani, inaitaka Serikali kutoa majibu kama watuhumiwa na ujangili wanafikishwa na kuondolewa pasipo kufuata taratibu za kisheria na kuwaachia huru,na huu ndio uthibitisho kwa watanzania jinsi tulivyo na Serikali iliyojaa rushwa na yenye kufumbia macho vitendo vikubwa vya rushwa hivyo watanzania kupoteza matumaini na  kukosa imani na vyombo vyao vya  dola hasa Jeshi la Polisi.
Mheshimiwa Spika, vilevile kumekuwepo kwa taarifa za majangili wa utafutaji masoko wa nyara za Serikali, wasambazaji wa silaha za kivita,wafadhili wa ujangili wenye wawakilishi wao na kufanya kazi ya kusambaza sumu ya kuulia wanyama,bunduki na risasi. Kambi rasmi ya Upinzani inahoji pamoja na taarifa hizi kuwepo upande wa serikali kwa majina na aina ya silaha zinazomilikiwa na watuhumiwa hawa na kutozifanyia kazi,serikali  itoe majibu ni mkakati gani uliopo kama sio Serikali inahusika katika ujangili huu?
Mheshimiwa Spika, usalama wa tembo uko hatarini kutokana na serikali kutochukua hatua dhidi ya ujangili wa tembo pamoja na taarifa za ujangili huo kuwepo serikalini na viongozi wa CCM kushiriki katika ujangili na kulindwa, mfano Mzee Lazaro ambaye ni Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Karatu, Yeye anamiliki silaha aina ya Rifle .375  akiwa ni mshirika wa mtandao wa ujangili kwa kuwepo vielelezo kuwa anashirikiana na BRYSON BALOSHINGWA ambaye Serikali imeendelea kumlinda. Kambi rasmi ya Upinzani inataka Serikali kwa kupitia Waziri husika kuwaeleza watanzania je ni sera ya Serikali ya CCM katika kufumbia macho masuala yanayotishia ustawi wa taifa kwa kuwalinda majangili wakiwemo viongozi wa CCM kama ambavyo tumetaja hapo juu ? Kwani pamoja na Serikali ya CCM  kuwa na  taarifa hizi bado imeendelea kuonyesha udhaifu wake katika kuchukua hatua za kisheria.
4.1 Utambuzi wa Majangili
Mheshimiwa Spika, pamoja na Bunge kukaa hapa na kupitisha bajeti za kuwezesha utendaji katika idara na Serikali, pamoja na idara kutimiza majukumu yake ya kuhakiki upatikanaji wa majangili ili wachukuliwe hatua bado zoezi hilo limeshindwa kufanyiwa kazi na Serikali. Hii ni dhahiri kwa Serikali ya CCM kuhusika na ubadhilifu wa maliasili za nchi hii na kuwahadaa wananchi kuwaletea maisha bora huku wakijinufaisha wenyewe na viongozi wake wa CCM hususani Mzee Lazaro ambaye ni Mwenyekiti wa CCM Karatu amabaye ametajwa katika orodha ya majangili wa tembo.
Mheshimiwa Spika ,Kambi rasmi ya upinzani inatoa rai kwa serikali kuruhusu TAKUKURU kuchunguza mazingira haya ya rushwa ikizingatiwa mgawanyo usio sawa Duniani umeonekana kuleta historia ya kuvuruga amani katika baadhi ya nchi,hivyo kufumbia macho vitendo hivi vitahatarisha amani ya nchi yetu.
Mheshimiwa Spika, katika moja ya ahadi  na utekelezaji wake Serikali iliahidi kuimarisha vituo vya doria katika eneo la KIA Nangurukuru na West Kilimanjaro. Kambi ya Upinzani inaitaka Serikali kusimamia utekelezaji wa sheria za utumishi wa umma na kuwezesha wafanyakazi kuheshimu mali za umma kwa kuzingatia wafanyakazi wa umma ndio hutumia fursa ya utumishi wao kuweza kuhujumu maliasili za nchi.
Mheshimiwa Spika,kukua kwa mtandao wa ujangili ulioenea karibu nchi nzima na kushamiri kwa usafirishaji wa nyara na silaha haswa za kivita na risasi za moto kupitia njia za maeneo ya Biharamulo,Kibondo,Kasulu, Kahama,na Urambo,Geita na Mpanda. Hii haihatarishi tuu usalama wa wanyama pia amani katika nchi kufuatia umiliki huu kuwa haramu.Kambi rasmi ya Upinzani inaitaka Serikali kutoa tamko juu ya hatua itakazochukua kukomesha ujangili kwa kutumia taarifa zilizopo ili iwe fundisho kwa wengine na kuiweka nchi katika mazingira yaliyo salama.
5.0 USALAMA WA FARU
Mheshimiwa Spika, pamoja na kuwa na ulinzi wa wanyamapori katika hifadhi, mwenendo wake unaendelea kutoleta matumaini kwa baadhi ya wanyama kuendelea kutoweka kwa kasi. Idadi ya faru waliokuwapo kwenye hifadhi miaka ya 1969 iliyokadiriwa kuwa kati ya 150 hadi 250 ilipungua hadi kufikia faru 20 miaka ya 1980. Kwa mujibu wa Mkurugenzi Mkuu wa TANAPA, Allan Kijazi, anasema, faru wa mwisho kuonekana katika hifadhi hiyo eneo la Pangalo ilikuwa ni mwaka 1985, huku faru wengine wote wakiteketezwa kwa kuuawa na majangili, ambapo idadi ya sasa ni 19 ikijumuishwa na watatu walioongezwa kutoka Uingereza na kufika  Tanzania Juni 17, 2012.
Mheshimiwa Spika, Kambi rasmi ya Upinzani inasikitishwa na kauli ya  Waziri Kagasheki alipokua akipokea Faru watatu kutoka Uingereza katika uwanja wa KIA kwamba majangili wanao mtandao mkubwa, wanazo pesa nyingi,swali ni je, hivi Serikali haina uwezo kifedha na kimtandao kuhakikisha inapambana na majangili hao ambao licha ya kuwa na mtandao mkubwa na uwezo kifedha pia wanazo silaha nzito za kivita?
Mheshimiwa Spika, Wakati wa vita kuu ya pili ya dunia kiongozi wa uingereza wakati huo Winston Churchill,aliwahi kusema “In every age there comes a time when a leader must come forward to meet the need of the hour, therefore ,there is no potential leader who does not have an opportunity to make a positive difference in the society.Tragically,there times when a leader does not rise to the hour. Katika tafsiri isiyo rasmi;
“Katika kila dahari hufika wakati anajitokeza kiongozi mwenye uwezo wa kuitikia mahitaji ya wakati huo. Hivyo kila kiongozi mwenye uwezo anayo fursa ya kuleta mabadiliko katika jamii. Kwa bahati mbaya kuna wakati amabapo kiongozi anashindwa kuitikia mahitaji ya wakati”.
Mheshimiwa Spika, inauma, inakera, inasikitisha na inaudhi kuona uongozi wa serikali ya CCM umeshindwa kuitikia hitaji la wakati huu ambalo ni kuwalinda wanyama wetu kwa gharama yoyote.Kambi rasmi ya Upinzani inachelea kuamini nguvu za majangili kuizidi Serikali,kama si Serikali kushirikiana na majangili,hivyo kuitaka Serikali kupitia shirika la hifahi za taifa TANAPA kuhakikisha usalama wa wanyamapori kwani ni wakati mwafaka kwa serikali kuamka na kuweka mipango madhubuti inayotekelezeka ya kuhakikisha ulinzi unaimarishwa dhidi ya faru na wanyama wengine wakiwamo tembo kwa kuishirikisha jamii inayoishi kuzunguka hifadhi zetu.
Mheshimiwa Spika, taarifa zilizopo Serikalini za ufuatiliaji wa tukio la kuuwawa kwa faru wawili (jike na mtoto) katika hifadhi ya Serengeti na taarifa hizi kuifikia menejimenti ya Shirika la Hifadhi za Taifa tarehe 17/5/2012. Uchunguzi ulibaini makundi maalumu mawili; Kundi la kwanza linahusisha wafanyabiashara, baadhi ya watumishi wa idara mbali mbali za Serikali kama vile Polisi, na Idara ya Wanyamapori (Game Reserves na Game scouts – watumishi wa Halmashauri) wanaoishi katika baadhi ya Wilaya hizo. Kundi la pili ni la Majangili/majambazi ambao hupatiwa silaha (bunduki), risasi na uwezeshwaji kifedha toka kwenye kundi la kwanza na baada ya kufanikisha, mazao yatokanayo na ujangili na ujambazi, huyauza au kugawana na wawezeshaji wao.
Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani inahoji pamoja na Serikali kuwa na taarifa hizi ni hatua zipi zilizochukuliwa kwa usalama wa hifadhi za taifa? Pia kuitaka Serikali kuheshimu rasilimali za nchi hii na kuwatendea haki watanzania kwa kuhakiki katika Serikali kulinda rasilimali kwa manufaa ya watanzania.
6.0 SITISHO LA USAFIRISHAJI WANYAMA NJE YA NCHI.
Mheshimiwa Spika, katika zoezi la kusitisha usafirishaji wa wanyama nje ya nchi Serikali iliendelea kufanya maamuzi yasio na tija kwa uchumi wa kitanzania kufuatia zoezi hilo kuhusisha biashara ya ndege wa aina zote na wale waharibifu kama kunguru, Ngedere, Tumbili na Reptilia, maamuzi haya yamepelekea kupoteza mapato ya serikali ambayo kwa mwaka 2008/2010 Serikali ilikusanya shilingi 408,724,551.00 hadi biashara inafungwa kwa kipindi cha mwaka 2011 Agosti 18, Serikali ilikua imekusanya shilingi 154,083,480.00.
Mheshimiwa Spika, haya ni maamuzi mabovu kwa Serikali yasiyozingatia athari katika uchumi wa nchi huku Serikali ikiendelea kutumia pesa nyingi kuteketeza wadudu waharibifu ambao wangeweza kutupatia mapato pamoja na kukuza ajira.Kambi rasmi ya Upinzani Bungeni inathubutu kusema utamaduni huu unazidi kukomaa na kuota mizizi kutokana na maamuzi ya kukurupuka yaliyofanywa na Serikali ya CCM. Hivyo, Kambi rasmi ya Upinzani, tunaitaka Serikali kurejea upya maazimio hayo na kuruhusu wadudu waharibifu waendelee kuuzwa nje badala ya kuteketezwa.
Mheshimiwa Spika, zoezi la kudhibiti kunguru weusi katika maeneo ya Kibaha,Morogoro na jiji la Dar Es Salaam kwa kutumia sumu aina ya DRC 1339 pamoja na mitego limeonekana kushindwa kwa kiasi kikubwa ikizingatiwa wingi wa kunguru hawa kuendelea kuwepo,Kambi ya Upinzani inaitaka serikali kulitafutia ufumbuzi makini kwa wakati kuondoa kero hii kwa kuruhusu wauzwe nje na wauzaji wasizuiliwe kuwakamata na kuwauza.

7.0 SEKTA NDOGO YA MISITU NA NYUKI.

Mheshimiwa Spika, Wakati Mhe.Waziri anazindua bodi ya ushauri ya Wizara ya Wakala wa Huduma za Misitu (TFS) Jijini Dar Es Salaam alithibitisha kuwa Tanzania inafilisiwa na viongozi wetu, kwa maana kuwa kuna ubadhirifu mkubwa wa mapato yanayotokana na maliasili zetu. Alisema nanukuu.... “jamani idara ya wanyamapori ina fedha nyingi, lakini zinaliwa na watu kwa maslahi binafsi na kama fedha hizo zingekuwa zinapelekwa serikalini kama inavyotakiwa, nchi hii kwa sasa ingefika mbali, mimi naogopa hata kutaja kiasi cha fedha hapa hadharani” .
Mheshimiwa Spika, Kwa nukuu hiyo toka kwa Waziri Mwenye dhamana, ni dhahiri kuwa sekta hii inauwezo mkubwa sana wa kuchangia kiasi kikubwa katika pato la Taifa na kiasi kingine kuachwa ili sekta iweze kujiendesha na kutengeneza mazingira ya kuwavutia wawekezaji wengi zaidi. Kambi rasmi ya Upinzani inataka kujua je ni mkakati gani ambao Waziri ameuandaa wa kubana mianya ya upotevu wa mapato uliokuwa unaendelea katika sekta hiyo? Na ni hatua gani za kisheria zimechukuliwa kwa watu wote waliohusika na ubadhirifu wa mapato kama ambavyo Waziri alibaini?
Mheshimiwa Spika,Ripoti ya Mthibiti na Mkaguzi Mkuu wa hesabu za serikali iliainisha upotevu wa pesa kwa kiwango cha shilingi 874,853,564 kutokana na kufanyika kwa maamuzi ya upendeleo kwa kutoa kiwango cha chini cha mrahaba kwa mauzo ya misitu.Hii ni uthibitisho wa kutosha wa kutoendelea kwa sekta ya misitu ikizingatiwa wenye mamlaka katika usimamizi wa rasilimali misitu wameshindwa kuzingatia maadili ya utumishi na sheria na kujilimbikizia mali kwa kupindisha taratibu za kiutendaji.
Mheshimiwa Spika,Kambi  rasmi ya Upinzani inaitaka Serikali kuchukua hatua thabiti za kuzuia upotevu huu kwa kuzingatia kuwa rasilimali za taifa hili zinapaswa kunufaisha watanzania wote na sio kikundi cha watu wachache ambao wamepewa dhamana ya kusimamia rasilimali hizo kwa niaba yetu sote.
Mheshimiwa Spika, ahadi ya Serikali  katika mwaka 2011/2012 ilitangaza  kuendelea kupitia na kuboresha Sera, Sheria, Kanuni na Taratibu pamoja na Programu za Misitu na Nyuki ili ziendane na wakati pamoja na kufanya tafsiri ya Kanuni za Misitu na Nyuki kutoka lugha ya Kiingereza kwenda Kiswahili na kusambaza nakala 4,500 kwa wadau mbalimbali. Kambi rasmi ya Upinzani inaitaka Serikali kuliambia Bunge hili mchakato huo umefikia wapi ? Na je wadau wameshirikishwa kwa kiasi gani mpaka sasa?

Mheshimiwa Spika, Serikali ilizungumzia swala la  kuongeza wingi na ubora wa mazao ya nyuki, ila utekelezaji wake hauoneshi dhamira ya Serikali katika kuongeza wingi na ubora wa mazao yatokanayo na nyuki kwa kutowekea mkazo katika uendelezaji wa shughuli za ufugaji nyuki kwa vitendo, na hasa katika kuongeza uhamasishaji kwa jamii kushiriki katika masuala ya misitu na ufugaji nyuki kwa  kutoa elimu ya utunzaji na matumizi bora ya rasilimali za misitu na nyuki kwa kufanya huduma za ugani na kusambaza majarida na vipeperushi.

Kambi ya upinzani , inaitaka serikali kuacha kutoa matamko kila siku na badala yake sasa wafanye kwa vitendo.

7.1 WAKALA WA HUDUMA ZA MISITU (TFS)

Mheshimiwa Spika, kutokana na matatizo ya mabadiliko ya tabia nchi kuendelea kushika kasi na kwa kuzingatia tatizo hilo kuendana na uvunaji wa misitu kwa kasi, hivyo wakala wa huduma za misitu pamoja na ahadi ya kuandaa mipango ya usimamizi wa hekta milioni 1.36 za misitu ya hifadhi ya uzalishaji (Misitu ya Asili na Mashamba 16 ya miti ya kupanda) kufuatana na mipango kazi ilivyopitishwa,Kambi rasmi ya Upinzani inaitaka Serikali kueleza mafanikio yaliyofikiwa mpaka sasa na kutoa mwongozo wa jinsi itakavyokabiliana na tatizo la uvunaji wa misitu unaoendelea kwa kasi.

Mheshimiwa Spika, moja ya matatizo katika usimamizi wa misitu ya hifadhi Tanzania ni pamoja na kutokua na mipaka iliyohakikiwa na kuainishwa rasmi,pia kutokuwepo kwa wasimamizi wa hifadhi hizo za misitu,Kambi rasmi  ya Upinzani inaitaka Serikali kutoa majibu ya utekelezaji kwa  kurejea ahadi yake hapa bungeni kupitia waziri husika juu ya kuhakiki mipaka, kuchora ramani na kutayarisha mipango ya usimamizi na kuhakikisha hifadhi zitakazohakikiwa zinapangiwa mameneja ili kuimarisha usimamizi.

7.2 MFUKO WA MISITU TANZANIA
Mheshimiwa Spika, utekelezaji wa ahadi ya Serikali Katika Mpango kazi wa mwaka 2011/2012, Mfuko wa Misitu Tanzania ulitenga takribani Shilingi 500,000,000.00 kuwezesha jamii kuanzisha na kuendesha miradi midogo ya jamii ambayo ni rafiki wa mazingira pamoja na uanzishaji wa vitalu vya miti na upandaji miti katika mashamba ya vikundi na watu binafsi. Kambi rasmi ya Upinzani inaitaka serikali kutoa maelezo ya kuthibitisha jamii ngazi ya vijiji zinanufaika na miradi hii ikizingatiwa mfumo uliotumika katika utoaji wa fedha zilizotengwa haukumlenga mwananchi wa chini na kuwanufaisha wachache katika asasi za kiraia hivyo kutofikia lengo la Serikali.
8.0 MIPAKA YA HIFADHI
Mheshimiwa Spika, moja ya vipaumbele katika ilani ya CCM ni kuwezesha jamii zinazozunguka maeneo ya hifadhi kunufaika na rasilimali za wanyamapori na misitu. Aidha,hali ilivyo kwa jamii inayozunguka hifadhi ni tofauti na ilivyoazimiwa katika mipango ya mgawanyo wa rasiliamali hizo na kuendelea kuwaneemesha wachache huku wananchi wakiendelea  kuwa maskini,mfano utanuzi wa mbuga ya Mpanga, wilayani Njombe kwa kuwatoa wananchi wa vijiji vilivyo karibu katika maeneo bila kulipwa fidia ya mashamba yao na maeneo yaliyokua malisho ya mifugo yao ni dhahiri uwekezaji huo hauna manufaa kwa wananchi wanaozunguka hifadhi na uendelea kuongeza lindi la umasikini uliokithiri
Mheshimiwa Spika,kumbukumbu za bunge zinaonesha kuwepo kwa tatizo katika meneo mengi juu ya kero za maeneo yenye hifadhi na mapori tengefu ,Mbunge wa Njombe magharibi mwaka 2009 februari alipokua akichangai bajeti ya Wizara alisema “Hoja yangu hapa ni juu ya uhai wa Wanyama na Uhai wa Wananchi, wanaoishi katika maeneo husika, kwenye jimbo langu katika Kata ya Luduga, Wilaya Njombe na pia Kata ya Wangama, Wilaya Njombe, wananchi wangu wanaishi kwa wasiwasi na mateso makubwa, juu ya kuongeza mipaka ya hifadhi ya Kipengere Mpanga Game Reserves. Mipaka ya zamani haina matatizo. Naomba kauli ya Serikali juu ya tatizo hili; ni lini ufumbuzi wa kudumu utafanyika?”.
Mheshimiwa Spika,majibu ya Serikali yalikua hivi , “Napenda kusema kwamba pori la akiba la Mpanga Kipengere, limeanzishwa kisheria kwa tangazo la Serikali la namba 483 la mwaka 2002 wakati zoezi la kuweka mipaka lilithibitika kwamba kuna baadhi ya vijiji vimo ndani ya hifadhi. Ili kutatua tatizo hilo Serikali itashirikiana na wadau kupitia upya mipaka hiyo ili kuhakikisha kuwa maeneo ya vijiji husika yanakuwa nje ya pori husika” .
Mheshimiwa Spika, pamoja Serikali kutozingatia ahadi yake na kutozingatia sheria ya Ardhi ya vijiji  Na.5  ya 1999, na kutothamini umuhimu wa wananchi wake katika kutumia ardhi,Serikali imeruhusu TANAPA kuongeza mipaka ya mbuga ya mpanga pasipo kuzingatia sheria ya ubadilishaji wa matumizi ya ardhi kwa kubadili mipaka ya  maeneo ya vijiji mfano kijiji cha Imalilo chenye usajili NA:350,Kata ya Wangama wilayani Njombe kuwa mbuga ya Mpanga pasipo kufuata taratibu ikiwa ni pamoja na kuwashirikisha wananchi katika mkutano mkuu wa kijiji na kuendelea kuwanyanyasa wananchi wa maeneo hayo pamoja na kutoza faini ya shilling laki tatu pindi waingizapo mifugo katika eneo hilo.
Mheshimiwa Spika, Kambi rasmi ya Upinzani inaitaka Serikali kuzingatia sheria katika kubadili matumizi ya ardhi kwa kuzingatia manufaa ya umma kama sheria inavyoelekeza na sio kuendelea na utamaduni wake wa sasa wa kuwanyanyasa na kuwadhulumu wananchi ardhi yao na kuwaacha bila kujua la kufanya.
9.0 SEKTA NDOGO YA UTALII
Mheshimiwa Spika,Kambi rasmi ya Upinzani ilitoa maelezo kwa Serikali katika kipindi cha bunge cha mwaka 2011/2012 kuhusu ya Wakala wa Usafirishaji Watalii, kifungu cha 58 kifungu kidogo cha (1) na (2), cha Sheria ya Utalii ya mwaka 2007, kwa ujumla wake vinaelekeza kwamba shughuli za uwakala wa kusafirisha watalii na kuongoza watalii mlimani zifanywe na Watanzania tu, Pia, kifungu cha 3 cha Sheria ya TANAPA ya mwaka 2003, kinaielekeza TANAPA kushughulika tu na Wakala wa Utalii aliyeandikishwa na mwenye leseni (za TALA) na ambaye ni mwanachama wa chama kinachoshughulika na masuala ya utalii.
Mheshimiwa Spika, Kambi rasmi ya Upinzani inaitaka Serikali kwa kuzingatia maslahi ya mtanzania katika shughuli za utalii kutoa maelezo ya utekelezaji wa sheria hii na usimamizi wake.Aidha hali ilivyo inaonyesha kampuni nyingi za kigeni zinafunguliwa hapa nchini kwa mbinu ya ubia kati ya wageni na watanzania wakati wenye kampuni hizo wanakuwa ni wageni, na hivyo wageni wanapata mwanya wa kufanya biashara ya utalii mlimani na faida kubwa inabaki nje badala ya kubaki kwa Watanzania.
Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani inaitaka Serikali kulieleza bunge ni hatua gani Serikali imechukua kuhakikisha Sheria ya Utalii ya mwaka 2007 inasimamiwa kwa manufaa ya Watanzania, ikiwa kampuni za wageni zilizokuwa zikifanya uwakala wa safari za mlimani bado zinaendelea kufanya kazi hiyo, licha ya sheria kutaka ifanywe na watanzania pekee? Na je, Serikali imechukua hatua gani dhidi ya kampuni za kigeni zinazoendelea kutumia mbinu ya kuingia ubia watanzania katika kufanya biashara ya utalii ya kupeleka watalii mlimani, ikiwa faida kubwa iliyopaswa kuwa ya watanzania inaendelea kwenda nje na kunufaisha kampuni hizo.

Mheshimiwa Spika ,Tanzania ni miongoni mwa nchi zenye vivutio vingi vya watalii duniani, ikiwa ni pamoja na hifadhi za wanyama, mlima Kilimanjaro, fukwe za bahari na kadhalika. Vivutio hivi vina mchango mkubwa katika ukuaji wa sekta ya utalii na uchumi wa taifa kwa ujumla lakini havijatangazwa kwa kiasi inavyostahili hivyo kuchangia katika uingiziaji mdogo na usioridhisha wa pato la utalii ukilinganisha na nchi jirani .


Mheshimiwa Spika, Sekta ya utalii Tanzania inategemea zaidi wageni kutoka nje ya nchi kitu ambacho kinaifanya sekta kuwa hatarishi kwa mabadiliko yanayotokea duniani,ikizingatiwa kuwa kushuka katika uchangiaji wa pato la taifa pale utokeapo msukosuko wa uchumi duniani pamoja na jitihada hafifu za Serikali katika kuhamasisha utalii wa ndani. Vilevile Sekta ya utalii pia inakabiliwa na vikwazo mbalimbali vikiwemo upungufu wa ujuzi katika nyanja za ufundi, uongozi na ujasiriamali wa ndani katika sekta ya utalii wa kisasa, miundombinu duni na huduma duni za kusaidia watalii (afya, fedha, bima, teknolojia ya mawasiliano na kadhalika).


Mheshimiwa Spika , Kambi rasmi ya Upinzani inaona ni dhahiri vikwazo hivi vimeifanya Tanzania kushindwa kutumia kikamilifu fursa zilizopo katika sekta ya utalii, ambazo zingechangia kwa kiasi kikubwa katika kukuza Pato la Taifa, hivyo Kambi rasmi ya Upinzani inaitaka Serikali kutengeneza mazingira yatakayo ruhusu utalii usio tegemezi hivyo ili kukuza utalii asilia,utalii tamaduni, utalii michezo na utalii makongamano/mikutano.


Mheshimiwa Spika, vilevile kikwazo kingine kikubwa katika utalii ni idadi ndogo ya hoteli isiyoweza kukidhi mahitaji ya wageni, mpaka sasa Tanzania tuna hoteli na camping sites 167 tu. Kiasi hiki ni kidogo sana ukilinganisha na idadi ya watalii wanaojaribu kufanya booking ya kuja kutaIii Tanzania wanaambiwa nafasi zimejaa, na hii inawafanya baadhi ya wenye hoteli kujipangia bei wanavyotaka na kuufanya utalii Tanzania uonekane ni gharama. Aidha kumekuwepo na malalamiko pamoja na tuhuma kuhusu baadhi ya watalii wa ndani hasa wenye ngozi nyeusi kutopewa huduma za malazi na chakula na kuwepo kwa utoaji kipaumbele kwa watanzania wenye asili nyeupe, hizi ni shutuma nzito za ubaguzi wa rangi ambapo Serikali inatakiwa kutoa majibu ya kina kuhususiana na shutuma hizi.


Kambi rasmi ya Upinzani inapenda kuishauri Serikali kutoa nafasi na vipaumbele kwa makampuni ya ndani yenye uwezo wa kuendesha sekta ya utalii kwa ufanisi na weledi. Kwa mfano katika mkoa wa Iringa kuna makampuni ambayo yameonyesha nia ya kuwekeza katika biashara za malazi na kukuza utalii kama MR Hotel, Tananka LtD, Hilltop Hotel, Kalenga Hotel, Embakassy Hotel, Mfugale (muekezaji anayejenga hoteli ya nyota tano), na familia ya Hanspop ambayo inajenga hoteli na shughuli za uwindaji pamoja na makampuni mengine mengi ambayo yamekuwa yakifanya biashara hii toka awali. Hii ni mifano ya watanzania ambao wameonesha nia na dhamira ya kukuza utalii hasa hasa ukizingatiwa kuwa utalii wa nyanda za juu kusini, hususani hifadhi ya taifa ya Ruaha inahitaji kutangazwa na kuliongezea taifa letu mapato.


10.0 BODI YA UTALII TANZANIA (TTB)


Mheshimiwa Spika, mambo ya msingi ambayo bodi ya utalii inahitaji kuyafanya ni pamoja na kuhakiki uendelezaji wa sekta ya utalii nchini. Hali ilivyo sasa sekta ya utalii imeendelea kukua zaidi katika mikoa ya kaskazini mwa nchi.Kambi ya Upinzani inaitaka serikali kupitia wizara ya maliasili na utalii kuandaa mpango yakinifu wa kuweza kutekeleza uendelezaji wa utalii kwa kuutangaza katika mikoa ya kusini na mashariki pamoja na maeneo ya pwani. Pia tunaishauri Serikali kupitia bodi hii kuendeleza mpango mkakati wa uhifadhi katika kupunguza msongamano wa kitalii kwenye korido ya mikoa ya kaskazini pekee na kuvutia utalii katika mikoa mingine yenye vivutio tosha.


Mheshimiwa Spika, Tanzania ni nchi iliyo kwenye viwango vya chini katika uendelezaji wa utalii wa ndani. Aidha, pamoja na kuwepo kwa program mbalimbali za kuhamasisha utalii wa ndani lakini bado elimu hii haijafanikiwa kuwafikia watanzania wengi kutembelea vivutio mbalimbali nchini na kukuza utalii wa ndani. Kambi rasmi ya Upinzani bungeni inaitaka bodi ya utalii kushirikiana na wadau wa utalii kuendeleza elimu ya uhamasishaji utalii wa ndani ili kuweza kubadili mitazamo ya watanzania na kuwawezesha katika kubadilika, kuthamini na kutumia bidhaa za utalii asilia.


11.0 MAMLAKA YA HIFADHI YA NGORONGORO.


11.1 Manunuzi ya Huduma Bila Mkataba Halali

Mheshimiwa Spika,Tatizo la kutokuwepo kwa mikataba halali kati ya Taasisi za Umma na watoa huduma na wauzaji bidhaa limeendelea kuwa kikwazo katika utekelezaji wa Sheria ya Manunuzi ya Umma ya mwaka 2004,Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro ambapo Mamlaka ilifanya biashara na wamiliki wa hoteli za kitalii na watoa huduma mbalimbali bila ya mkataba,Kambi rasmi ya Upinzani inaitaka serikali kusimamia sheria ili kuepuka mazingira kama haya yaliyo na harufu za rushwa.

Mheshimiwa Spika,katika taarifa ya Mthibiti  na Mkaguzi Mkuu wa hesabu za serikali ilibainisha kuwa Mamlaka ya Hifadhi ya Bonde la Ngorongoro ilifanya malipo kabla ya kupokea mali (advance payment) ya kiasi cha Shilingi milioni 643.76 kwa Toyota Tanzania Ltd mwezi Aprili, 2008 kwa ajili ya ununuzi wa magari,Katika kiasi kilichotolewa magari yenye thamani ya Shilingi milioni 471.3 yaliletwa mnamo tarehe 15 Agosti 2008 na mengine yenye thamani ya Shilingi milioni 137.9 tarehe tarehe 30 Juni 2010,Hivyo kiasi cha shilingi milioni 34.4 kati ya fedha zilizolipwa kwenye fedha za awali hazijarejeshwa kwenye mamlaka takribani miaka mitano sasa.


Mheshimiwa Spika, mpaka sasa kwa taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa hesabu za Serikali inaainisha kuwa hakuna makubaliano juu ya jinsi fedha zitakavyorejeshwa,Huu ni uvunjifu wa sheria za usimamizi wa fedha za umma ambapo imeelezwa wazi kwamba fedha zisilipwe kwa wauzaji wa bidhaa au huduma kabla ya kupokea mali na kama makubaliano ya mkataba yanaruhusu basi ni muhimu zirejeshwe ndani ya kipindi cha miezi 12.


Mheshimiwa Spika, Kama muuzaji au mtoa hudhuma atashindwa kutimiza wajibu wake, kinyume cha hapo adhabu kali inapaswa kutolewa. Kambi rasmi ya Upinzani inaitaka Serikali kutoa majibu ya jinsi inavyoshughulikia suala hili mpaka sasa na imechukua hatua gani.


11.2  Bodi za Wakurugenzi wa NCAA Kuingilia Kazi za Menejimenti.


Mheshimiwa Spika, Kambi rasmi ya Upinzani ilihoji katika hotuba yake ya mwaka 2011/2012, pia taarifa ya mkaguzi na mdhibiti mkuu wa hesabu za serikali amethibitisha wajumbe wa bodi ya mamlaka ya hifadhi ya ngorongoro wakijihusisha katika utendaji wa kazi za menejimenti. Kitendo hiki ni kasoro kubwa na inapunguza uhuru wa menejimenti kutoka kwa bodi na inaleta migongano ya kimaslahi kati ya pande hizi mbili taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi  Mkuu wa hesabu za Serikali ilithibitisha namna ambavyo bodi ya wakurugenzi ilivyojihusisha mara kadhaa katika maonyesho ya kimataifa ya utalii katika kipindi kati ya Julai, 2010 na Juni, 2011.


Mheshimiwa Spika, Hali hii ni kinyume na utawala bora na waraka wa Ikulu No. SHC/B.40/6/21 wa tarehe 28/03/1994 aya ya 3 na 5. Utaratibu huu huathiri kazi za bodi za usimamizi kwa kuwa zitakuwa zimegawanyika kimtazamo na kimaslahi.


Mheshimiwa Spika, pamoja na Kambi rasmi ya Upinzani kuishauri serikali na kuhakikisha tume ya kuchunguza bodi ya Ngorongoro ikiwemu mwenyekiti wa bodi ambaye ni makamu mwenyekiti wa CCM taifa Mh Pius Msekwa, sasa ni zaidi ya siku mia tatu sitini na tano na robo yani mwaka, tume hiyo imeshindwa kuleta ripoti ya uchunguzi ili ifanyiwe kazi,na bado serikali imeendelea kujiita serikali sikivu.


Mhjeshimiwa Spika, Kambi rasmi ya Upinzani inaamini itakapotokea kutotekelezwa majukumu ya kiutendaji yaliyotolewa kwa wajumbe wa bodi, Wajumbe wa Bodi hawatakuwa na nguvu ya kufuatilia na kudai maelezo juu ya kushindwa kufikiwa kwa malengo hayo, na hivyo bodi itabaki kufanya maamuzi yanayolinda maslahi yao katika utendaji wa mamlaka husika na huu sio utawala bora.


11.3 Kukosekana kwa Miongozo ya Utendaji wa Bodi ya mamlaka ya Ngorongoro.

Mheshimiwa Spika,Miongozo ya utendaji wa bodi (charter) ni maandiko yanayowaelekeza wajumbe wa bodi kwenye Shirika na mwelekeo wake na ambayo inafanya kazi kama mwongozo wa kiutendaji wa bodi kwa kutoa taarifa juu ya muundo wa bodi na utendaji ikiainisha kazi na majukumu ya wajumbe wa bodi. Pia, inajumuisha miongoni mwa mambo mengine kanuni za maadili ikiwemo sera ya migongano ya kimaslahi, sera ya uhudhuriaji wa vikao vya bodi, mwongozo wa kutathmini kazi za bodi, miongozo ya kutathmini utendaji wa mkurugenzi mkuu, historia za wajumbe wa bodi, kalenda ya bodi na mpango kazi wake,

Mheshimiwa Spika,Kambi rasmi ya Upinzani inaamini ukosefu wa mwongozo huu yaweza kueleweka kuwa bodi husika haina mwelekeo katika kuendeleza malengo ya mamlaka hivyo kujali maslahi binafsi kama ilivyothibitishwa katika taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa hesabu za serikali ya mwaka 2010/2011. Taarifa hiyo imebaini mamlaka ya hifadhi ya Ngorongoro(NCAA) haikuandaa mwongozo wa bodi (Board Charter) na hivyo kujiweka katika mashaka ya kukosa mwongozo wa utendaji kazi.


12.0 Hitimisho.


Mheshimiwa Spika, nimalizie hotuba yangu kwa maneno ya baba wa taifa Mwl.Nyerere aliyoyasema 1962 kuwa “Watu walio hatari sana ni wale ambao wanafikiri kuwa wa najua Kila kitu, wala hawana haja ya kujifunza zaidi. Hii ni tabia mbaya ambayo huzuia Mendeleo. Sababu moja iliyotuzuia sisi waafrika kuendelea ni majbu rahisi kwa matatizo makubwa. Shamba letu Kama halikutoa mavuno ya kutosha, jibu lilikuwa wazi: au limelogwa au ni amri ya Mungu. Watoto wetu walipokuwa wagonjwa Damian, jibu lilikuwa rahisi: au wamerogwa au ni amri ya Mungu. Nyumba ilipopigwa radi ikaanguka, jibu lilikuwa rahisi uchawi au amri ya Mungu”.


Mheshimiwa Spika, Majibu ya namna hii huzuia binadamu kupata sababu za kweli za matatizo yao, yanazuia akili kutafuta njia za kweli na za uhakika  za kuyaondoa matatizo hayo.
Siku hizi, tumeanza kutumia Majibu mengine ya rahisi, mambo yakienda mrama, badala ya kutumia akili zetu na kutafuta sababu za kweli, tunawalaumu wazungu,au wahindi,au ukoloni,au ukoloni mpya au vibaraka n.k. Lakini yafaa akili ifikie jibu hilo baada ya uchunguzi wa kweli,  sio uvivu wa kutumia akili. Uvivu wa kutumia akili unaweza kutufanya tutumie dawa kuondoa matatizo ambayo si dawa hata kidogo. Nikienda kwa daktari anitibu maradhi yangu, natazamia kuwa kazi yake ya kwanza ni kujua hasa sio kwa kubahatisha naumwa nini, kazi yake ya pili ni kujua sababu ya ugonjwa wangu. Daktari asipoujua ugonjwa wangu na sababu zake huwezi kujua dawa yake. Akinipa dawa nikapona atakuwa kaniponya kwa Bahati tu, kwa desturi daktari wa namna hiyo haweza kumponya mgonjwa, na udaktari wake ni wa hatari sana.


Mheshimiwa Spika, Kadhalika chama ambacho nia yake ni kuwa daktari wa matatizo ya jumuiya hakinabudi kiwe na tabia ya kujua matatizo yenyewe, sababu ya matatizo hayo na dawa yake. 
Ni wakati muafaka kwa serikali kuhakikisha inatambua matatizo yaliyopo katika wizara hii na kutafuta tiba vinginevyo serikali kuwa wazi mbele ya   watanzania kuwa imeshindwa na kukiuka kile alichokiamini baba wa taifa kwa serikali, ni vema Waziri  awe wazi kama  ameshindwa kutatua  matatizo haya ndani ya Wizara aseme ili aweze kupatiwa dawa stahiki .

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo kwa niaba ya kambi ya upinzani naomba kuwasilisha.


.............................


Mchungaji Peter Msigwa

Mbunge wa Iringa Mjini
Msemaji Mkuu wa Kambi ya Upinzani
Wizara ya maliasili na Utalii









No comments:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...